Katika kuhakikisha shule za sekondari zinakuwa na vyumba vya maabara za masomo ya sayansi na si maabara tuu bali maabara zenye vifaa, serikali kupitia programu ya Lipa kutokana na matokeo 'P4R' imetoa shilingi milioni 480 kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu ya shule za msingi na sekondari,ikiwemo maabara.
Kupitia fedha hizo, halmashauti ya Arusha inatekeleza miradi ya ujenzi, umaliziaji na ukarabari wa maabara za masomo ya Sayansi kwenye jumla ya shule 9 za sekondari.
Shule ya sekondari Oldonyosambu ni miongoni mwa shule hizo tisa ambayo maabara tatu za masomo ya Fizikia, Kemia na Biolojia zinafanyiwa ukarabati.
Mkuu wa shule ya Oldonyisambu, mwalimu Leshai Moita amesema kuwa ukarabati huo unaendelea kwa vyumba vitatu vya maabara, unaohusisha uwekaji wa mifumo ya maji na gesi pamoja ukarabati mdogo wa majengo ambao utagharimu kiasi cha shilingi milioni 15 kwa milioni tano kwa kila chumba.
Mkuu huyo wa shule ameongeza kuwa, ukamilishaji wa maabara hizo, utarahisisha tendo la kufundisha kwa mwalimu na kujifunza kwa mwanafunzi na kupandisha kiwango cha taaluma shuleni hapo.
Diwani wa kata ya Oldonyosambu, mheshimiwa Raymond Rairumbe, licha ya kuridhishwa na ukarabati huo amekiri kuwa kukamilika kwa maabara hizo kumeanza kuamsha morari ya wanafunzi kupenda masomo ya Sayansi, tofauti na hapo awali wanafunzi waliyachukia masomo hayo kwa kuyaona ni magumu.
Ameongeza kuwa, sehemu kubwa ya tendo la kujifunza linahusisha vitendo, kwa asilimia 75 ya tendo zima la kujifunza huku asilimia 25 pekee zikihusisha kusikia na kuona.
"Kuwepo kwa maabara kutasaidia wanafunzi kujifunza kwa nadharia na vitendo, jambo litakalomwezesha mwanafunzi kujiamini kwa kile anachojifunza, kukumbuka na zaidi kulipenda masomo ya Sayansi, masomo yanayotegemewa kutupeleka kwenye uchumi wa kati ifikapo 2025". amesema mheshimiwa Lairumbe
Hata hivyo wazazi na walezi wanatakiwa kufuatilia mara kwa mara, maendeleo ya kitaaluma ya watoto wao wawapo shuleni, jambo linamhamasisha mwanafunzi kuona umuhimu wa elimu wanayoipata na si kuwaachia walimu peke yao.
Pichani ni majengo matatu ya maabara ya Kemia, Fizikia na Biolojia sekondari ya Oldonyosambu.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.