Na. Elinipa Lupembe.
Zoezi la kufanya tahmini ya matokeo makubwa sasa (Big Result Now 'BRN'), kwenye vituo vyote vya kutolea huduma za afya halmashauri ya Arusha limekamilika, huku halmashauri hiyo ikifanikiwa, kupata matokeo mazuri ukilinganisha na matokeo mabaya, ya mwaka uliopita.
Zoezi hilo limefanyika kwa takribani siku kumi, na kufanikiwa kutembelea na kukagua, jumla ya vituo 55 vya kutolea huduma za afya vya serikali na vya binafsi, ikiwemo hospitali, zahanati na vituo vya afya.
Kiongozi wa timu iliyofanya tathmini hiyo, Dkt. Peter Neema, amesema kuwa, matokeo ya tathmini kwa mwaka huu ni mazuri zaidi ukilinganisha na matokeo mabaya ya mwaka uliopita, ambapo vituo vingi vilipata nyota sifuri.
Dkt. Peter amefafanua kuwa, jumla ya vituo 9 vya kutolea huduma za afya mwaka huu vimepata nyota tatu *3 huku vituo viwili tu, vikipata nyota sifuri *0 kati ya vituo 55, vilivyofanyiwa tathmini wakati mwaka jana ni vituo vitatu tuu vilipata nyota tatu.
Aidha Dkt. Peter, amewataka wahudumu wa afya kujitahidi kufanyakazi kwa weledi na kuzingatia kanuni na taratibu za utoaji, huduma za afya ili kufikia malengo yaliyowekwa na serikali ya vituo vyote kuwa na nyota 3 mpaka 5.
"Kuna mambo yanayopimwa yasiyohitaji fedha wala gharama bali ni weledi wa mtoa huduma, ikiwemo costomer care, namna ya utoaji huduma bora, uandikaji na utunzaji wa data, ujazaji wa fomu za ophras kwa watumishi, mambo hayo yote yako ndani ya uwezo wa muuguzi, hivyo ni vema wakayazingatia ili kufikia malengo yaliyopangwa "amesema Dkt. Peter.
Naye daktari katika hospitali ya halmashauri wilaya ya Arusha Olturumet, Dkt. Ester Luhunga amesema kuwa, licha ya matokeo hayo kuwa si ya kuridhisha sana, lakini matokeo hayo yameboreka sana kulinganisha na mwaka uliopita.
Aidha Dkt. Luhunga, amesema kuwa kufuatia matokeo hayo, halmashauri imeweka mikakati na kujipanga upywa tena kwa tathmini ijayo kwa kuhakikisha vituo vyote vinafuata taratibu za utoaji huduma kulingana na maelekezo hasa kwa mambo yaliyo ndani ya uwezo wa watumishi katika vituo.
Dkt. Luhunga, ameendelea kufafanua kuwa, changamoto kubwa iliyowakosesha kupata alama kuanzia tatu ni pamoja na zahanati nyingi kutokuwa na maabara na kushindwa kutoa vipimo vya magonjwa ya msingi, sambamba na upungufu wa watumishi katika vituo vingi vya kutolea huduma za afya.
" Tunaandaa mpango wa kibajeti wa kuwa na angalau chumba cha maabara katika zahanati zetu, hata kuweza kupima vipimo vichache ili kufikia malengo ya serikali ya kutoa huduma za matibabu kwa magonjwa ya msingi, karibu na wananchi" amefafanua Daktari huyo
Hata hivyo, Muuguzi wa halmashauri ya Arusha, Violeth Chahe, amesema kuwa wanategemea kufanya vizuri zaidi hasa kwenye mambo yaliyo ndani ya uwezo wa wauguzi, kwa kuboresha mapungufu madogo madogo yaliyojitokeza wakati wa ukaguzi.
" Tumeachiwa mpango kazi na Timu ya wizara, ambao una mwongozo wa mambo yote muhimu ya kuzingatia katika utoaji huduma bora, kupitia mwongozo huo ni lazima tathmini ijayo tutafanya vizuri na kufikia malengo" amesema Chahe
Timu hiyo ya kufanya tathmini, imefafanua lengo la kufanya tathmini hiyo ni pamoja na kuboresha utoaji wa huduma bora za afya na kufikia asilimia 80% ifikapo mwishoni mwa mwaka huu wa 2018, na endapo kituo hakitafikisha kinaweza kuwa kwenye hatari ya kufungiwa.
Timu hiyo pia imeainisha, jumla ya viashiria 12 vinavyopimwa vikiwa vimegawanywa kwenye makundi manne ambayo ni utoaji huduma bora kwa mgonjwa au mteja ikiwa ni pamoja na mpangilio wa huduma tangu kufika mpaka kuondoka kwa mgonjwa.
Pia, uwepo wa huduma baada ya kumgonjwa kumuona daktari yani vipimo vya maabara, X- ray, huduma ya upasuaji, upatikanaji wa dawa, masuala ya rufaa kwa wagonjwa pamoja na huduma za dharura, uwepo wa miundo mbinu sahihi na bora na upatikanaji wa vifaa tiba, usimamizi na utawala bora katika vituo vya kutolea huduma za afya ni mambo ambayo lazima yapatikane kwenye kituo chochote cha kutolea huduma za afya.
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.