Na Elinipa Lupembe.
Viongozi wa mila wa kabila la kimaasai nchini Tanzania, wamekubaliana kuungana na serikali na asas zisizo za serikali, kupinga ukatili wa kijinsi kwa wasichana, ukatili uliofanya na kabila hilo kulingana na mila na desturi za kabila hilo.
Viongozi hao wa kimila, maarufu kama Malaigwanani, wamekiri kukomesha tabia za tohara kwa watoto wa kike pamoja na kuozesha watoto katika umri mdogo,na kukubaliana kuwaacha watoto hao wasome kama ilivyo malengo ya serikali na haki za mtoto pia.
Hayo yamethibitishwa na Katibu wa mila za kimaasai Tanzani, Mzee Amani Lukumai, alipokuwa akizungumza na wananchi kwenye Bonanza la Mtoto wa Kike, liliofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Bangata halmáshauri ya Arusha.
Katibu huyo wa mila, aliyevuta hisia za watu wengi, ameweka wazi kuwa katika kikao, cha Malaigwanani, kilichofanyika siku za hivi karibuni, wamekubaliana kuachana na mila hizo potofu, mila zinazomkandamiza mtoto wa kike, badala yake wameahidi kumsimamia mtoto wa kike, aweze kupata haki zake za msingi ikiwa ni pamoja na elimu.
"Sisi viongozi wa mila ya kimaasai nchini, tumepitisha azimio la kuungana na serikali yetu, kumtetea mtoto wa kike kutokana na ukatili dhidi yake, kwa kuhakikisha tohara zinakomeshwa, hakuna ndoa za utotoni, hakuna kumchagulia mtoto mchumba, badala yake tutamsimamia mtoto wa kike asome" amesema katibu wa mila, mzee Lukumai.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji, halmashauri ya Arusha, wakati wa kufunga Bonanza hilo, Afisa Maendeleo ya Jamii, halmashauri hiyo, Angela Mvaa, amewasisitiza, watoto wa kike kutumia fursa walioyonayo ya kuwa shuleni, kuzingatia masomo, kwa kuwa wazee na wazazi wao wamekubali kuachana na mila na desturi zao, na kuwaacha wasome.
"Ni wasihii wasichana, wazazi wenu wamekubali kuachana na mila za tohara na ndoa za utotoni, wamekubali kuwatetea na kuwaacha msome, tumieni fursa hiyo, kusoma kwa bidii ili muweze kutimiza ndoto zenu, fursa ambayo wasichana wengi wa kabila la kimaasi waliikosa, tambueni mna bahati elekezeni juhudi zenu kwenye masomo" amesisitiza Angela
Namnyaki Salekwa mwanafunzi wa shule ya msingi Ilkiding'a, amewashukuru viongozi hao wa mila, kwa kukubali kuwatetea watoto wa kike, kwa kuwa mila hizo zilizuia wasichana wengi, kuendelea na masomo, na hata wengine kushawishiwa kufanya mitihani vibaya ili wafeli waolewe, na wengine kubeneshwa mimba na kutoroshwa, wangali wanafunzi.
"Tumefurahi kusikia wazee wetu, wameamua kuachana na mila hizo potofu za kumkandamiza mtoto wa kike, mila zilizowaumiza na kuharibu ndoto za mtoto wa kike, kwa vile wameamua sasa tusome, hatuta waangusha, tutasoma kwa bidi ili tuwathibitishie wazee wetu maamuzi waliyoyafanya sahihi kwa mtoto wa kike"amesema Namnyaki
Naye Mkurugenzi wa shirika la Center for Women and Children Development (CWCD), Hindu Mwego, amesema kuwa, baada ya mapambano ya muda mrefu dhidi ya ukatili kwa mtoto wa kike, hatimaye jamii imeanza kuelewa, huku hali ya ukatili kwa mtoto wa kike ikianza kupungua, licha ya changamoto nyingi lakini wanaamini kwa kushirikiana na viongozi wa mila kuendeleza mapambano iko siku, mila hizo potofu zitatokomea kabisa.
Hindu ameongeza kuwa, uwepo wa Bonanza hilo liliowakutanisha watoto, licha ya kuwapatia watoto burudani na jumbe zenye mafunzo, limeambatana na maonesho ya shughuli za mikono wanazozifanya watoto shuleni wakiwa kwenye klabu zao za kupinga ukatili dhidi ya Mtoto wa kike, klabu ambazo zinasimamiwa na walimu kwa udhamini wa shirika la CWCD la mjini Arusha.
Bonanza hilo la mtoto wa Kike, limeandaliwa na halmashauri kwa kushirikiana na shirika la CWCD, kwa ufadhili wa shirika la Foundation for Civil Society na kuwakutanisha wanafunzi wa shule 14 za msingi na sekondari za halmashauri ya Arusha, likiwa na lengo la kumjengea uwezo mtoto wa kike kujiamini, kujithamini ili kuweza kulinda na kutetea haki zake dhidi ya ukatili wa mtoto wa kike.
PICHA ZA MATUKIO YA BONANZA
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.