Na. Elinipa Lupembe.
Halmashauri ya Arusha imejipanga kuwachukulia hatua za kisheria wazazi ambao, wanaharibu ushahidi wa kesi za ukatili dhidi ya watoto wa kike na kuamua kumalizana nyumbani kifamili huku watoto wao wakikosa haki zao, kutokana na ukatili wanaofanyiwa na watu wao wa karibu ndani ya jamii.
Hayo yamethibitishwa na mkurugenzi mtendaji halmashauri yaa Arusha, Seleman Msumi, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa kike, yaliyofanyika kwenye viwanja vya shule ya msingi Ilboru kata ya Ilboru.
Mkurugenzi Msumi ametoa tamko hilo mara baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa Watoto wa Kike, waliofika kwenye maadhimisho ya siku yao hiyo muhimu, kupitia jumbe mbalimbali zilizowasilisha kwa njia ya sanaa za nyimbo, ngonjera, mashairi, pamoja na risala iliyosomwa kwa mgeni rasmi, wakielekeza malalamiko yao kwa wazazi kuwa ni chanzo cha kuharibu kesi za watoto kwa kukukubali kukaa na watuhumiwa na kumalizana kimila jambo ambalo linawakera watoto na zaidi kuwanyima haki zao, ambazo Serikali kupitia vyombo vya mbalimbali wamekuwa wakijitahidi kusimamia.
Aidha mkurugenzi huyo ameiasa jamii na wazazi kuacha mara moja tabia hiyo, tabia ambayo kwanza ni dhambi lakini pia licha ya inawakosesha watoto haki zao, na kuwafanya watoto kuwa wanyonge na kushindwa kujiamini mbele ya jamii huku wakiendelea kukatizwa ndoto zao, kutokana na wazazi kushindwa kuwasimamia.
"Wazazi tunajukumu kubwa la kuwalinda watoto wetu, pamoja na malezi, jukumu kubwa zaidi ni kuwalinda watoto wetu wasifanyiwe vitendo vya ukatili, pamoja na kusimamia haki zao pale inapotokea mtoto wa kike amefanyiwa ukatili wa aina yoyote, wazazi tusirudi nyuma kutokana na rushwa ama kulinda undugu wa familia zetu"
"Niwahakikishie katika kipindi cha uongozi wangu, nitapambana na wazazi wenye tabia ya kutaka kuharibu kesi yoyote ya mtoto kwa kujaribu kumaliza kesi hizo kinyumbani, zaidi niahidi nitasimamia haki za mtoto, nitasimamia na kufuatilia kesi zilizopo na zitakazojitokeza dhidi ya ukatili kwa watoto na kuhakikisha watoto wanapata haki zao na si vinginevyo" amesisitiza Mkurugenzi huyo.
Hata hiyo kiongozi wa katibu wa mila na Katibu wa Malaigwanani, mkoa wa Arusha, Aman Lukumai, ameweka wazi kuwa kwa sasa jamii ya kimaasai imeanza kubadilika, na matukio ya ukatili kwa watoto wa kike kupitia mila za kabila la kimaasai, zimeanza kupungua, wazazi wengi wameanza kuelewa umuhimu wa kumuendeleza mtoto wa kike kwa kumuacha asome tofauti na huko nyuma ambapo mtoto wa kike alionekana ni wa kuolewa tuu, na kusababisha ndoa na mimba za utotoni.
"Sisi kama viongozi wa mila, tunaungana na serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali kuelimisha jamii ya kimasaai, kuachana na mila potofu zinazo mkandamiza mwanamke na zaidi mtoto wa kike, lakini pia tukiendeleza tamaduni zinazojenga maadili katika jamii, niiombe serikali kupitia mkurugenzi na watalamu, katika mapambano dhidi ya ukatili kwa watoto, endeleeni kutoa elimu kwa jamii ya kimasaai, jamii ambayo haikuwa na ufahamu mkubwa juu ya umuhimu wa mtoto wa kike kusoma, lakini kutokana na mkakati wa kuwaelimisha, ninaamini iko siki ukatili huo dhidi ya wanawake na watoto utatoweka kabisa" ameweka wazi Laigwanani huyo.
Naye Mkurugenzi wa shirika la Center for Women and Children Development (CWCD) Hindu Mwego, licha ya kuishukuru serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake za kumkomboa mtoto wa kike lakini ameiomba serikali kufanya mambadiliko ya baadhi ya vifungu vya sheria ambavyo bado vinamkandamiza mtoto wa kike na kusistiza kuwa sheria hizo zimepitwa na wakati.
"Kuna baadhi ya vifungu vya sheria za kimahakama na za polisi zimekuwa kikwazo katika upatikanaji wa haki ya mtoto hata kama ushahidi uko wazi kwamba mtoto amefanyiwa vitendo vya ukatili"
Maadhimisho hayo ya Siku ya Mtoto wa Kike Kimataifa yalipambwa na sanaa za nyimbo, mashairi, maigizo, ngonjera pamoja na maonesho ya kazi mbalimbali za mikono zinazofanywa na Watoto wa Kike, yakiwa yameandaliwa na halmashauri ya Arusha kwa kushirikiana na Shirika la Center for Women and Children Development (CWCD) kwa ufadhili wa shirika la Foundation For Civil Society ( FCS), maadhimisho yaliyobeba Kauli mbiu ya "KIZAZI CHA KIDIGITALI, KIZAZI CHETU"
Sekei Road
Anuani ya posta: 2330 Arusha
Simu : +255 027 2502737
Simu: 073 65000476
Barua pepe: ded@arushadc.go.tz
Copyright ©2018 Arushadc . All rights reserved.